16 November 2015

YAFICHUKA HII NDIO SABABU YA Sitta, Nchimbi kukatwa uspika.


Hatimaye mchuano wa uspika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) umechukua sura mpya baada ya vigogo kadhaa kutemwa wakiwamo spika wa zamani, Samwel Sitta na aliyewahi kuwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Dk. Emmanuel Nchimbi.
Naibu Spika wa Bunge la 11, Job Ndugai, Naibu Mwanasheria Mkuu, Dk. Tulia Ackson na Mbunge wa Afrika Mashariki, Abdullah Ali Mwinyi ambaye ni mtoto wa Rais Mstaafu Ali Hassan Mwinyi ‘Mzee Ruksa’ ndiyo waliopenya katika mchujo uliofanywa na Kamati Kuu ya CCM jana, huku vyanzo mbalimbali vikitaja suala la umri na makundi kuwa ni miongoni mwa sababu zilizowaponza waombaji wengine 20 waliojitosa katika mbio hizo. Makada 23 wa CCM ndiyo waliokuwa wakiwania uspika kumrtihi Anna Makinda aliyetangaza kustaafu.
Katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika Oktoba 25, mbali na kushinda nafasi ya urais iliyotwaliwa na Dk. John Magufuli, CCM pia ilifanya vizuri ubunge baada ya kutwaa majimbo 186 na hivyo mgombea yeyote atakayepitishwa na chama hicho kuwania uspika atakuwa na nafasi kubwa ya kushinda dhidi ya wapinzani ambao kwa ujumla walitwaa majimbo 74.
Bunge la 11 linatarajiwa kuanza kesho na Rais Magufuli anatarajiwa kulizindua Ijumaa.

MCHUJO ULIVYOKUWA 
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Dodoma jana, Katibu wa CCM wa Halmashauri Kuu ya Taifa, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, alisema Kamati Kuu (CC) ya chama chao ilikuwa na kikao maalum chenye ajenda moja tu ya kuwapitisha wagombea wa nafasi ya spika.
Aliwataja Ndugai, Dk. Tulia na Abdulla Mwinyi kuwa ndiyo waliopitishwa kuwania nafasi hiyo na mchakato wa kumpata mgombea mmoja utaanza leo.
“Kamati Kuu imewateua wanachama wa CCM watatu ambao wanapelekwa katika kamati ya wabunge wa CCM kesho (leo) kwenda kuchaguliwa mmoja ili awe mgombea wa uspika wa bunge,”alisema Nape.
Nape alisema majina ya watatu hao yatawasilishwa kwenye kamati ya wabunge wa CCM leo saa 4:00 asubuhi makao makuu ya chama hicho mjini Dodoma na kupigiwa kura huku mmoja atakayeshinda kati yao ndiye atakayepelekwa bungeni kuchuana na mgombea wa upinzani kuwania kiti hicho.
Kuhusu nafasi ya Naibu Spika, Nape alisema ratiba iliyotolewa juzi na chama hicho ilikosewa kwa bahati mbaya kwani nafasi hiyo itashughulikiwa na kamati ya wabunge wenyewe wa CCM.
“Sasa kwa mujibu wa kanuni za Chama Cha Mapinduzi, suala la Naibu Spika halishughulikiwi na kamati kuu bali na kamati ya wabunge wa CCM,”alisema Katibu huyo.
Alifafanua kuwa kanuni za CCM, toleo la nne la mwaka 2011, ibara ya 57, inasema mwanachama wa CCM anayetaka kugombea nafasi ya Naibu Spika wa Bunge atajaza fomu maalum ya maombi na kuiwakilisha kwa katibu wa kamati ya wabunge wote wa CCM katika muda ambao umewekwa.

“Ada ya fomu hiyo ni shilingi laki moja ambazo zitatolewa wakati akirudisha fomu kwa katibu wa kamati. Kwa hiyo suala la Naibu Spika kutoka CCM litamalizwa na kamati ya wabunge wa CCM,” alisema Nape.

Kadhalika, alisema kwa mujibu wa ratiba, wabunge wa CCM wanaotaka kugombea nafasi hiyo watachukua fomu kuanzia leo (Novemba 16) na kuzirudisha kesho kabla ya saa 10:00 jioni.

Aliongeza:”Uchaguzi utafanywa na wabunge wa CCM na unategemewa kufanyika tarehe 17 (kesho) kumpata mgombea mmoja wa nafasi ya unaibu spika.


KILICHOWAPONZA

Vyanzo mbalimbali viliiambia Nipashe jana kuwa miongoni sababu zilizowapa nafasi Ndugai, Mwinyi na Dk. Tulia ni kutokuwa na makundi, ujuzi wa masuala ya sheria na pia umri.

Kadhalika, imeelezwa kuwa mbali na sababu hizo, vigezo vingine vinavyodaiwa kuzingatiwa ijapokuwa havikutajwa wazi ni pamoja na jinsia na pia umuhimu wa kuwa na sura ya muungano walau katika nafasi tatu za wagombea.

Ndugai ana uzoefu wa kutosha kwani ndiye aliyekuwa Naibu Spika wa Bunge la 10, Abdullah ni kijana ambaye pia ana uzoefu na masuala ya Bunge kwani hadi sasa ni Mbunge wa Afrika Mashariki na pia anatokea Zanzibar. Kwa upande wa Dk. Tulia, yeye ni msomi kijana aliyezaliwa mwaka 1976 na aliwahi kufanya vizuri wakati alipokuwa Mjumbe katika Bunge Maalum la Katiba.

Chanzo kimoja kimeiambia Nipashe kuwa kwa kuzingatia mambo hayo na mengine kadhaa yanayohusiana na sifa za kawaida walizokuwa nazo makada wote waliojitosa kuwania uspika, huenda ndiyo maana Sitta na Nchimbi wakawa miongoni mwa wale walioachwa katika orodha ya wagombea watatu wa mwisho.

“Sitta ana uzoefu mkubwa kuhusiana na masuala ya Bunge. Ni wazi kwamba umri wake wa takriban miaka 70 unaweza kuwa sababu mojawapo ya kukosa nafasi hii kwani vinginevyo, ni wazi kwamba naye asingekosekana katika orodha ya wagombea watatu wa mwisho,” chanzo kimoja kiliiambia Nipashe kuhusiana na kuenguliwa kwa Sitta ambaye inaelezwa kuwa alizaliwa mwaka 1942, zaidi ya miaka 70 iliyopita.

Kadhalika, kuhusiana na kukatwa kwa Nchimbi, chanzo kingine kiliiambia Nipashe kuwa waziri huyo wa zamani atakuwa ameponzwa na makundi ndani ya chama, hasa kutokana na ukweli kuwa kwa muda mrefu iliaminika kuwa yeye alikuwa katika kambi ya Edward Lowassa ambaye alienguliwa katika mbio za urais ndani ya CCM kabla ya kuhamia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).

Imeelezwa kuwa Nchimbi ambaye ni miongoni mwa wajumbe wa Kamati Kuu (CC) ni msomi na tena hana umri mkubwa kama Sitta, lakini kitendo chake cha kukana maamuzi ya CC wakati alipoenguliwa Lowassa wakati wa mbio za urais ndicho kilichomponza.

“Ni wazi kwamba Nchimbi ameponzwa na hisia za baadhi ya watu kwamba bado yeye ni mtu wa karibu wa Lowassa… vinginevyo, ni wazi kwamba naye asingekatwa kirahisi,” chanzo kiliiambia Nipashe.

Mbali na Sitta na Nchimbi, makada wengine wa CCM waliokuwa wakiwania nafasi ya uspika ni pamoja na Gasbert Blandes na mawaziri wa zamani , Balozi Philip Marmo na Ritta Mlaki.
Akizungumza kwa njia ya simu, Sitta alisema bado hafahamu chochote juu ya kukatwa kwake.
“Sijaarifiwa. Siwezi kuzungumza chochote kwa kitu nisichokijua, sijasikia na kawaida ninavyojua huwa tunaitwa na kuambiwa kasoro… hivyo sijui sababu za kuondolewa kwangu. Inabidi tusubiri kwanza,” alisema Sitta.

Miongoni mwa wagombea wa nafasi hiyo walioenguliwa, Banda Sonoko, alisema yeye binafsi anapongeza mfumo uliotumika kupata majina hayo matatu na hivyo anamuunga mkono yeyote atakeyepitishwa na Kamati ya Wabunge wa CCM kuwa mgombea.
Mbunge mteule wa Chunya (CCM), Victor Mwambalaswa, alisema ni kanuni na taratibu za chama zilizotumika kuwachuja na kuwapitisha wagombea watatu na kwamba, uamuzi huo unadhihirisha kuwa ndani ya CCM hakuna kiongozi mkubwa wala mdogo bali wanachama wote wana hadhi sawa.

Mbunge mteule wa Viti Maalum (CCM), Mkoa wa Mbeya, Dk. Mary Mwanjelwa, alisema CCM inaongozwa kwa sheria na kanuni na hivyo maamuzi yaliyotolewa na kikao cha kamati kuu yanapaswa kuheshimiwa, bila kuangalia ni kina nani wameenguliwa.

Mbunge mteule wa Nkasi Kaskazini, Ally Kessy, alisema majina yaliyopitishwa na kamati kuu yamezingatia jinsia, muungano na sifa za kila mmoja.

“Hakuna mtu maarufu. Wote ni maarufu, mfano Mwinyi ni Mbunge wa Afrika Mashariki, Dk. Tulia ni Naibu Mwanasheria Mkuu na Ndugai alikuwa Naibu Spika katika Bunge la 10. Wote waliopitishwa wana sifa zinazostahili,” alisema Kessy.

Mbunge mteule wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu, alisema mchakato huo utakuwa umetumia vigezo ambavyo yeye havifahamu lakini, kama ni Ndugai atapitishwa, basi ni janga kwani alikuwa Naibu Spika wa Bunge la 10 ambaye alishindwa kuendana na kasi ya bunge.

Kuhusiana na Dk. Tulia, alisema inasitikisha ,kwani ameshindwa kutimiza kiapo cha utumishi wa umma na kujiingiza kwenye siasa. Kuhusu Abdullah, alisema anaamini kuwa umarufu wa baba yake, Rais mstaafu Mwinyi, umemsaidia kupata nafasi hiyo.

Akizungumza na Nipashe jana, Mwenyekiti wa Umoja wa Wanataaluma katika Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOMASA), Nashoni Maisori, alisema kwa maoni yake, Sitta hakupaswa kupewa nafasi ya kugombea tena uspika kwani kuongoza kwake Bunge Maalum la Katiba kulitosha kumuondolea sifa.

Mkuu wa Chuo cha Biashara (Aseki), Omary Kiputiputi, alisema kukatwa kwa Sitta, Nchimbi na vigogo wengine CCM ni jambo la kawaida kwani ndivyo demokrasia ilivyo na kwamba, wengine walishatumikia serikali kwa muda mrefu na sasa ni wakati muafaka kwao kupumzika na kulijenga taifa kupitia maeneo mengine.

Mkazi wa Area C mkoani Dodoma, Gerald Simon, alisema kwa upande wake, anaamini Sitta ndiye mtu sahihi aliyepaswa kupitishwa na CCM na hivyo anashangaa kusikia ameenguliwa.


CHANZO:NIPASHE

No comments:

Post a Comment

Comments system

Disqus Shortname