14 March 2015

Kinana Afunguka Urais ..Lowassa safi, Nyalandu Anazurura Tu


Jana ilikuwa siku ya hisia tofauti kwa watu wawili wanaotajwa kwenye kinyang’anyiro cha urais, Edward Lowassa na Lazaro Nyalandu baada ya Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana kumsifu mmojawao na kumponda mwingine.

Akiwa Kondoa, Kinana alitumia muda mwingi kujibu kilio cha wananchi wanaosumbuliwa na askari wa wanyamapori kwa kumponda Waziri Nyalandu kuwa anazurura bila kushughulikia matatizo ya wananchi, lakini saa chache baada ya kuwasili Monduli alimsifu Lowassa kuwa ni kiongozi shupavu.

Tayari Nyalandu ameshatangaza nia ya kugombea urais, wakati Lowassa, mmoja wa wanachama wa CCM wanaotajwa sana kwenye kinyang’anyiro hicho, hajatangaza uamuzi wake lakini anatumikia adhabu ya chama chake kilichomfungia kujihusisha na harakati za uongozi pamoja na makada wengine watano.

Baada ya msafara wa Kinana kuwasili Monduli na kupokewa na viongozi wa chama hicho wa eneo, katibu huyo wa CCM, Kinana alipata nafasi ya kuzungumza machache kabla ya kuanza safari ya kukagua shughuli mbalimbali.

“Hatuna shaka na Monduli kwa kuwa yupo kiongozi shupavu, ndugu yetu Waziri Mkuu mstaafu na mjumbe wa (Halmashauri Kuu ya CCM) Nec,” alisema Kinana akiwaelezea wananchi waliokuwapo eneo hilo.

“Wa Monduli mna kiongozi shupavu na mchapakazi. Hongera Bwana Lowassa.”

Baadaye, Lowassa aliwakaribisha akisema: “Mmefanya kazi kubwa sana ya kukijenga chama chetu. Nawashukuru sana, karibuni.”

Naye katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alisema: “Nafurahi kuwa katika jimbo la mzee wangu, rafiki yangu Edward Lowassa. Mapokezi mazuri, bila shaka Arusha mmeamka.”

Kinana amekuwa akitumia sehemu kubwa ya ziara yake kushuhutumu viongozi wa Serikali na hasa mawaziri kwa kushindwa kuwatatulia wananchi matatizo yao na ilifikia wakati aliwataja mawaziri wanne aliowaita kuwa ni mizigo, tofauti na alivyofanya kwa waziri mkuu huyo wa zamani.

No comments:

Post a Comment

Comments system

Disqus Shortname