25 July 2012

MSHTAKIWA WA EPA NA MWENZAKE JELA MIAKA 18


MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam, imemhukumu kifungo cha miaka 18 jela Kada wa CCM, Rajabu Maranda na binamu yake, Farijala Hussein katika kesi ya tuhuma za kuchota Sh2.2 bilioni za Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) ndani ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT). Mahakimu wawili
katika jopo la waliokuwa wakisikiliza kesi hiyo waliwatia hatiani watuhumiwa kwa makosa sita kati ya saba yaliyokuwa yakiwakabili na kuwahukumu kifungo cha miaka mitatu jela kwa kila kosa. Kwa upande wake kiongozi wa jopo hilo, Jaji Fatuma Masengi aliwaachia huru washtakiwa hao kwa maelezo kwamba upande wa mashtaka ulishindwa kuthibitisha mashtaka yote saba yaliyokuwa yanawakabili. Hata hivyo, hukumu hiyo haikuweza kuwaokoa watuhumiwa na hasa Farijala na Maranda watatumikia adhabu yao kwa miaka mitatu jela kwa kuwa adhabu zote walizopewa zitakwenda kwa wakati mmoja. Tayari Maranda na Farijala wanatumikia kifungo kingine cha miaka mitano jela, baada ya kupatikana na hatia ya wizi wa Sh1.8 bilioni za EPA, ambapo walihukumiwa na mahakama hiyo Mei 23, 2011. Jopo lagawanyika Jopo la mahakimu watatu lililokuwa likisoma hukumu hiyo liligawanyika na kusoma hukumu mbili tofauti, ambapo hukumu moja iliyoandaliwa na kusomwa na kiongozi wa jopo hilo, Jaji Masengi aliyewaachia huru washtakiwa. Hata hivyo, katika hukumu ya pili, iliyoandaliwa na Hakimu Projestus Kahyoza na mwenzake Catherine Revocate iliwatia hatiani washtakiwa katika makosa sita kati ya saba yaliyokuwa yakiwakabili, na kuwahukumu kifungo cha miaka mitatu kwa kila kosa. Hata hivyo, wakati wakisoma hukumu hiyo, mahakimu hao walisema badala ya washtakiwa kutumikia kifungo cha miaka 18, hukumu yao itaenda sambamba hivyo watatumikia kifungo cha miaka mitatu jela. Kabla ya hukumu Kabla ya hukumu hiyo kutolewa, hakimu Kahyoza na mwenzake walipitia ushahidi uliotolewa na mashahidi sita wa upande wa  mashtaka  akiwamo mtaalamu wa maandishi, Joseph Mgendi ambaye aliweza kuangalia saini katika nyaraka halisi na zinazodaiwa kughushiwa,  ikiwamo hati ya usajili  ambapo alibainisha kuwa zilikuwa zimeghushiwa. Pia walipitia utetezi uliotolewa wa mshtakiwa Maranda, ambaye aliyakana mashtaka yote saba yanayowakabili na kwamba, alikataa katakata kuwa hakuwahi kula njama na kughushi hati ya usajili wa Kampuni ya Money Planners & Consultant. Hakimu Kahyoza alisema, Maranda alidai kuwa yeye hakuwahi kwenda Brela kusajili kampuni hiyo na kwamba, aliyewahi kwenda kusajili kampuni ni binamu yake, Farijala. Hakimu Kahyoza alisema, Maranda katika utetezi wake alisema yeye hakuwahi kughushi hati yoyote hivyo, haikuwa rahisi kwake kutoa hati iliyoghushiwa pia, hakuwahi kuiba fedha BoT na wala hakuwahi kujipatia fedha yoyote kwa njia ya udanganyifu. Kahyoza alifafanua kwamba, Maranda alidai mfumo uliotumika kuwaingizia fedha kwenye akaunti yao iliyopo katika Benki ya CBA uliendeshwa kihalali ndiyo maana, BoT hawakuwahi kulalamika hivyo, aliiomba mahakama imuone hana hatia. Akisoma utetezi uliotelewa na Farijala, Hakimu Kahyoza alisema, Farijala naye alikataa  madai ya kughushi, kuwasilisha nyaraka bandia benki, kuiba fedha yoyote na kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu na aliiomba mahakama imwachie huru kwa sababu hana hatia. Yasiyo na utata Hakimu Kahyoza alisema kuwa mahakama ilibaini kuwapo kwa masuala yasiyokuwa na utata ambayo ni pamoja na kwamba Maranda na Farijala ni ndugu, waliwahi kufanya biashara pamoja na waliingiziwa fedha kwenye akaunti namba 0101379004 ya United Bank of Africa ambazo ni kiasi cha Sh2.2 bilioni. “Baada ya kuweka msingi huo, mahakama ilijiuliza je, washtakiwa walikula njama ya kuiibia  BoT, walighushi hati ya usajili wa kampuni namba 150731, walighushi hati ya mkataba kati ya Kampuni ya Money Planners & Consultant  na Kampuni ya B. Grancel ya nchini Ujerumani, waliwasilisha nyaraka za kughushi benki, waliibia BoT na kwamba je, walijipatia fedha kwa njia ya udanganyifu,” alihoji Kahyoza. Hakimu huyo alisema kwa kuzingatia ushahidi uliotolewa,  hakuna utata kuwa hakuna mahali panapoonyesha washtakiwa ndiyo walikuwa wamiliki wa kwanza wa kampuni hiyo Money Planners & Consultant na kwamba majina yanayodaiwa kuwa ni wamiliki wa kampuni  hiyo ya Thobias  Kitunga na Paulo  ni majina ya uongo na ya kufikirika. Alisema licha ya majina hayo kuwa ya kufikirika, mabadiliko ya kampuni hiyo ya Money Planners & Consultant hayakuwahi kufanyika na hata Brela hakuna kumbukumbu, hivyo saini zilizopo katika nyaraka za kampuni hiyo ikiwamo hati ya usajili ni za kughushi. Alisema sababu ya kuthibitisha hilo ni kwamba, ofisi ni ileile iliyopo Magomeni Mapipa, Mtaa wa Iramba nyumba namba 7 hata baada ya mabadiliko. “Hati hizo za usajili hazikusainiwa na Msajili wa Biashara toka Brela, Noel Shani bali zilisainiwa na washtakiwa wenyewe. Hivyo, kwa mujibu wa kifungu cha 333 na 335 (c) (e) vimetufanya tufikie hitimisho kuwa  washtakiwa walighushi nyaraka hizo,” alisema Hakimu Kahyoza. Alisema Maranda na Farijala walighushi hati ya mkataba ya Septemba 8, 2005, wakitumia majina ya Thobiasi na Paul na kwamba hati hiyo haikusainiwa na Kampuni ya Money Planners & Consultant. “Maombi ya kupewa fedha hizo Sh 2.2 bilioni,  yalipitiwa na watu kadhaa wakiwamo Mwanasheria wa BoT na  kupeleka kibali cha mwisho kwa Gavana aidhinishe malipo, hakuna hata mmoja aliyebaini kuwa katika hati ya mkataba kati ya Kampuni ya B. Grancel ya nchini Ujerumani na Kampuni ya Money Planners & Consultant, haikuwa na saini ya Kampuni ya  Money Planners & Consultant,” alisema. Aliongeza: “Kwa sababu hiyo inaonyesha wazi, washtakiwa ndiyo walighushi  nyaraka hizo hivyo hati ya usajili  wa kampuni hiyo, hati ya mkataba ni za kughushi.” “Tuna haki ya kuamini kuwa washtakiwa kwa kujua, walifanya hivyo kwa nia mbaya ya kuwasilisha hati hizo za kughushi CBA na baadaye BoT”, alisema Kahyozi. Alisema hakuna ubishi kuwa hakuwapo hata shahidi mmoja aliyewahi kuthibitisha kuwa washtakiwa hao waliwahi kuiibia BoT Sh 660,210,000. “Katika hili hatupo tayari kukubaliana na upande wa mashtaka kwa sababu halijathibitika”. Aliongeza kwamba, hakuna utata kuwa BoT iliweka kwenye akaunti ya washtakiwa zaidi ya Sh2.2 bilioni na kwamba, kiwango hicho cha fedha kiliwekwa baada ya washtakiwa kuwasilisha hati za kughushi katika benki hiyo kuu ikiwamo hati ya usajili  na hati ya mkataba. Hakimu alisema kulikuwapo na maofisa wa juu BoT waliotakiwa walithibitishe hilo, lakini, Mwanasheria wa BoT yeye alikuwa anathibitisha uhalali wa hati hiyo ya mkataba ambayo haikusainiwa upande mmoja na Kampuni ya Money Planners kuwa, “Ina nguvu kisheria hivyo, inaweza kutumiwa  na BoT kuhamisha au kuchukua fedha zinazoongelewa  katika maombi ya washtakiwa”. Alifafanua hakimu, “Mwanasheria alimaanisha kuna watu wengine walithibitisha, sisi kwa mtazamo wetu ni ajabu kwa maofisa  hao hata mmoja hakuwahi kuona katika hati ya mkataba hakuna saini ya Kampuni ya Money Planners. Tunajiuliza walimezwa katika huu mtego au walipumbazwa? Kama walipumbazwa, upumbazo huo ulikuwa ni wa hali ya juu na kujikuta wote wanaingia kwenye mtego huu.” alisema Hakimu Kahyoza. Aliongeza kwamba washtakiwa hao walifanya matendo hayo yote kwa nia mbaya na kuwafanya watu wengine, wawe sehemu ya kughushi. Kuhusu shtaka la kula njama, kwa ujumla maelezo yote yanaonyesha  Maranda na Farijala, walikubaliana  makazi ya ofisi yawe Magomeni, Mtaa wa Iramba nyumba namba 7 ambako ni nyumbani kwao, waliwasiliana, walikutana, walijadiliana  hivyo walitenda kosa la kula njama. “Sisi hatuna sababu za kusitasita kuwa kweli washtakiwa walikula njama dhidi ya BoT. Ni kweli walikula njama,” alisisitiza Kahyoza. Jaji Masengi Kwa upande wake, Jaji Masengi aliwaachia huru washtakiwa wote kwa sababu upande wa mashtaka ulishindwa kuyathibitisha mashtaka yote saba yanayowakabili. Jaji Masengi alisema BoT ndiyo wangekuwa walalamikaji wakuu, lakini haikuwahi kulalamika kutoa fedha hizo zinazodaiwa kuibwa na washtakiwa wala Kampuni ya B. Grancel ya nchini Ujerumani. Kuhusu kughushi, alisema ushahidi uliotolewa haukutosheleza kuthibitisha kosa hilo na kwamba licha ya utetezi kuwa na upungufu lakini hakukuwa na sababu za kuwatia hatiani. Kabla ya hukumu Kabla ya kusomwa kwa hukumu ya Hakimu Khayoza na Hakimu Catherine, Wakili wa Serikali, Alapha Msafiri aliiambia mahakama kuwa washtakiwa siyo wakosaji wa mara ya kwanza, wanatumikia kifungo cha miaka  mitano jela katika kesi namba 1161 ya mwaka 2008. Msafiri aliiomba mahakama itumie kifungu cha 348 na 358 cha Makosa ya Jinai (CPA), kutoa amri Maranda na Farijala walipe fidia au warejeshe kiasi walichojipatia kwa njia ya udanganyifu. Wakili Majura Magafu, anayewatetea Maranda na Farijala, alidai kuwa ni kweli washtakiwa walitiwa hatiani  lakini, isiwe kigezo  cha  kuwapa adhabu kali kwa sababu kesi namba 1163 na 1161 zilifunguliwa  siku moja, zinahusu makosa ya aina moja isipokuwa zilipangiwa jopo tofauti. “Hii ni tofauti na mtu aliyetenda kosa akaachiwa halafu akafanya tena kosa lingine, pia mazingira ya mashtaka yanayowakabili washtakiwa yalikuwa na utata kwa namna moja au nyingine na kwamba washtakiwa walitenda makosa bila ya kujua kama wanatenda makosa,” aliwatetea wakili huyo na kuongeza: “Kwa hiyo ni dhahiri, matukio hayo hayakufanyika kwa makusudi kwa asilimia 100, kwa kuwa wao waliamini ni halali lakini baadaye ilibainika kuwa si halai”. “Waheshimiwa washtakiwa wote wana matatizo ya kiafya, Farijala ana matatizo ya presha ya macho na Maranda ana tatizo la Figo, naomba kama mahakama itaridhia chini ya kifungu cha 38, ina mamlaka ya kuangalia mazingira ya utendwaji wa matukio, hali za watuhumiwa   na kuwaachia kwa masharti maalumu kutokana na afya zao,”alisema Magafu. Pia aliiomba mahakama itamke wazi wazi kuwa adhabu watakayopewa washtakiwa kama itakuwa ni ya kifungo, inastahili kuanza lini kwa sababu kumekuwapo na utata wa sheria, kuwa ni lazima wamalize kifungo cha awali ndiyo waanze kingine. Kwa upande wa Hakimu Catherine Revocate, alisema wamejadiliana  kwa kuangalia mazingira ya kesi, afya za washtakiwa  na kwamba ni wakosaji wa mara ya kwanza kwa sababu kesi hiyo inasimama peke yake, katika shtaka la kwanza hadi la saba kasoro shtaka la sita waliloachiwa huru; washtakiwa hao watatumikia kifungo cha miaka mitatu katika kila kosa.

No comments:

Post a Comment

Comments system

Disqus Shortname