07 November 2013

PICHA: MWIZI WA PIKIPIKI AFUNGIWA KWENYE BODABODA NA KUBURUZWA UMBALI WA KILOMITA MOJA KISHA KUCHOMWA MOTO.



Polisi wakiondoka na mwili wa marehemu
MTU mmoja asiyefahamika jina wala makazi yake, amepoteza maisha baada ya kupigwa na kuchomwa moto na wananchi ambao wameamua kujichukulia sheria mkononi.
Wananchi hao ambao ni wakazi wa eneo la Mtakuja Mbalizi, walifanya tukio hilo jana majira ya saa mbili asubuhi.
Mwenyekiti wa Kijiji cha Mtakuja Mbalizi Mbeya vijijini, Ambonisye Masinga, alisema kuwa  marehemu huyo alidaiwa kuiba pikipiki  eneo la Utengule.
Alisema, baadhi ya madereva wa bodaboda(pikipiki) walianzisha msako na kufanikiwa kumtia nguvuni marehemu huyo na kuanza kumshushia kipigo huku mwili wake ukiwa umefungwa kwenye pikipiki na kuuburuza barabarani umbali wa kilomita moja.
Alisema, mwili huo uliburuzwa na kufikishwa kwenye eneo la mlima reli maarufu kwa jina la eneo la adhabu kwa wahalifu  na kuchoma moto mwili wake.
Aidha, katika tukio hilo fundi ujenzi aliyekuwa katika eneo hilo Asangalwisye Mayasu(50) mkazi wa kivukoni, alijikuta akiambulia kipigo baada ya kujaribu kuwazuia wananchi ambao waliamua kujichukulia sheria mkononi.
“Baada ya msamalia huyu kupigwa na kuumizwa vibaya serikali ya kijiji ilimkimbiza hospitali Teule ya ifisi na kwamba hali ya afya yake si nzuri hali iliyopelekea mke wake aitwaye Kristina Kyando (45) Kuzirai,”alisema
Hata hivyo Kamanda wa Polisi mkoa wa Mbeya, Diwani Athumani, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba jeshi la polisi litahakikisha linawatia mbaroni watu wote waliohusika na mauaji hayo.
Kumeibuka kwa vitendo vya madereva  pikipiki kujichukulia sheria mkononi ambapo hivi karibuni walifunga barabara ya Iwambi Jijini Mbeya kwa kulishinikiza jeshi la polisi kuwaachia watuhumiwa wawili ambao  walituhumiwa kuiba pikipiki ili wawaue

No comments:

Post a Comment

Comments system

Disqus Shortname