12 July 2012

John John Mnyika awasilisha ushahidi wizi BoT !!!

Hatimaye Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika, amewasilisha ushahidi wa awali kwa Katibu wa Bunge, kuhusu tuhuma alizozitoa bungeni dhidi ya Mbunge wa Iramba Magharibi (CCM), Mwigulu Nchemba, kwamba ni mmoja wa watuhumiwa katika kashfa ya ukwapuaji wa mabilioni ya fedha uliofanywa katika Akaunti ya Malipo ya Nje (Epa) ndani ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT).

Hatua hiyo imechukuliwa na Mnyika kutekeleza maelekezo aliyopewa na Mwenyekiti wa Bunge, Jenista Mhagama, ambaye alimpa siku saba kuwasilisha ushahidi kuthibitisha kauli yake hiyo.

Kauli hiyo ilitolewa na Mnyika katika kikao cha Mkutano wa Bunge unaoendelea hivi sasa mjini hapa, kilichofanyika, Julai 3, mwaka huu, katika mjadala kuhusu makadirio ya mapato ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma. Siku hizo ziliisha juzi.


Kwa mujibu wa Mnyika, ushahidi huo aliuwasilisha kwa Katibu wa Bunge, mjini hapa juzi.


“Kuhusu tuhuma dhidi ya Mwigulu Nchemba, ushahidi wa awali nilishawasilisha leo (juzi) ndani ya siku saba kama ilivyotakiwa,” alisema Mnyika.


Katika mkutano huo uliotawaliwa na mvutano, malumbano, hisia kali na maneno ya kashfa miongoni mwa wabunge, Mnyika pamoja na mambo mengine, alisema Nchemba aliwahi kuwa mtumishi wa BoT, ambayo ilikumbwa na kashfa hiyo na kwamba, naye ni mmoja wa watuhumiwa.


Kauli hiyo ya Mnyika ilimfanya Mhagama kusimama na kumpa Mnyika siku hizo awe amewasilisha ushahidi wa kauli yake.


Kwa upande wake, Nchemba wakati akichangia mjadala wa Bunge, alisema alijiunga na BoT mwaka 2006 wakati huo ukwapuaji wa fedha BoT ulikwishafanyika.


Kwa upande wake, Kaimu Katibu wa Bunge, John Joel, alithibitisha kuwasilishwa kwa barua ya maelezo ya Mnyika.


“Ni kweli tumepokea jana barua ya maelezo lakini Spika atawaelezeni kesho (leo),” alisema.


No comments:

Post a Comment

Comments system

Disqus Shortname