16 March 2015

Aina tano za kuachana katika uhusiano

 
Yako baadhi ya uhusiano ambayo huwa yana vipindi vya amani kwa kitambo kidogo na milipuko ya ugomvi kwa kipindi kingine. Milipuko hii simaanishi kule kutoelewana kwa kawaida bali uhusiano unaokumbwa na milipuko ya kutoelewana kwa kitu fulani kizito au ugomvi, unakuwa mzito na wenye kuyumbisha pande zote mbili.

1. Kuchemka hadi kumwagika “The Boil Over”

Katika hali hii unaanza kuziona dalili za kuachana kwenu kwa mbali. Labda mwenzako amekuwa akifanya au kusema vitu fulani kwa muda mrefu na vimekuwa havikufurahishi, kila unapotaka kumpasukia kuna kitu kinakwambia “subiri, mpe nafasi nyingine”, ndani yako unajiona kabisa kuwa wakati umewadia sasa wa kumpasha habari yake kwa mara ya kwanza na ya mwisho. Pia ndani yako unakuwa na utayari wa kubeba majukumu kwa chochote utakachomwambia. Ghafla siku moja kinatokea kitu kidogo tu, labda ni neno lililosemwa au kitu kilichofanywa na wewe au mpenzi wako, mnagombana na kutofautiana sana na kutokana na machungu na maumivu ya muda mrefu moyoni mmoja anaamua kuutumia upenyo huo kulitamka neno “it’s over” (naomba tuachane) na huo unakuwa mwisho wa penzi lenu.

2. Kuachana kimlipuko

Yako baadhi ya uhusiano ambayo huwa yana vipindi vya amani kwa kitambo kidogo na milipuko ya ugomvi kwa kipindi kingine. Milipuko hii simaanishi kule kutoelewana kwa kawaida bali uhusiano unaokumbwa na milipuko ya kutoelewana kwa kitu fulani kizito au ugomvi, unakuwa mzito na wenye kuyumbisha pande zote mbili. Kwa mfano baada ya kitambo cha amani na mapenzi kunagundulika kuwapo kwa uhusiano wa pembeni kwa mmoja wa wapenzi (cheating) na hili linazua mlipuko wa ugomvi ambao ghafla unalizima penzi na ule ukaribu wenu unafifia ghafla na kutokomea jumla. Yamkini ni mlipuko mmoja tu umetokea, lakini mpenzi mmoja aliyeumizwa hatamani hata kumwona mwenzake kwa macho, wapendanao hawa wanajeuka maadui ghafla (one blow away).

3. Leo nje kesho ndani, kesho baridi keshokutwa moto

Hii ni staili ya kuachana ambayo wengi wetu huitumia mara kwa mara na mara nyingine pasipo mhusika mmoja katika penzi kufahamu kwamba safari ya kuachana ndo inawadia. Katika uhusiano wa watu wa namna hii, kunakuwa na mazingira yanayowafanya leo wanakorofishana kesho wanapatana, kesho wanakuwa pamoja keshokutwa unaskia hawapo tena pamoja, mara unasikia wamerudiana, tena wanakuja kufarakana na tabia hii inakuwa ndo maisha yao ya kila siku na mfumo wa uhusiano yao. Tabia hii huendelea kudumu hadi inafika nyakati mmoja akitoka basi anatoka jumla, kila mwenzake akiwaza kwamba yamkini atarudi kama mazoea yao yalivyo lakini haiwi hivyo tena na penzi lao linakatikia hapo.

4. Mkate ulioungua

Mara nyingi tunapopika mkate huuweka kwenye joto kali ili uive na mara kwa mara muokaji huuangalia kama umeiva kwa kuutumbukizia kitu kikali kama vile uma ili kuangalia hali yake ya ndani ilivyo na kufahamu maendeleo ya uivaji wake. Mkate uliosahaulika kuangaliwa mara kwa mara huungua na muokaji anapokuja kuutoboa ndipo anapofahamu kuwa mambo yameshaharibika kuanzia ndani na mkate haufai kuliwa tena.

Katika uhusiano wetu hususani kwa baadhi ya wale walioweza kukaa muda mrefu au hata waliooana, bahati mbaya kwa sababu ya masumbufu ya maisha ya kila siku na mapenzi ya kimazoea wakasahau kuchochea na kuziamsha hamasa za penzi lao kila mara, penzi hilo taratibu hushuka na kupoa ladha na taratibu pasipo wapendanao hawa kugundua kila kitu kinakuwa chabaridi, kilichoganda, kisicho na ladha na kilammoja akitamani penzi la ladha ya tofauti kutoka kwa mtu wa tofauti. Hii inasasababisha wawili hawa kuchagua kuachana.

5. Ghafla moto ghafla baridi

Kama umewahi kutumia mashine ya kupashia joto chakula “microwave” utaelewa kitu ninachojaribu kuzungumza hapa, tabia ya mashine hii ni kupasha joto chakula kwa haraka sana na mara kikitoka huweza kupoa kwa haraka zaidi pia. Yako mapenzi ambayo yameanzishwa ghafla sana (kwa muda mfupi sana) na yakapaa juu sana, kila mmoja akimhisi mwenzake kiukaribu sana, na hisia za wawili hawa zinakuwa za moto kama zilizo wekwa kwenye ‘microwave’ lakini ghafla mmoja kati ya wapendanao hawa anazimika na kutoendeleza tena moto uliokuwepo. Kwa mfano mlianza ghafla kuhusiana na mapenzi yakawa moto kuliko mlivyofikiri, kila siku mko wote na lazima muonane au muwasiliane kwa simu, ghafla mwenzako hapokei simu na wala akiiona simu yako hawajibiki kukupigia au kukwambia nini kinaendelea na tabia hiyo inaendelea hivyo hivyo hadi unakata tama na unaamua kukubali yaishe.

Mapenzi haya yaliwaka na kuzima kwa mtindo wa microwave. Wakati unahisi penzi lenu linafikia mwisho ni vyema mkafikiri njia bora za kuachana na maranyingine ikibidi kuliongea hili kwa pamoja. Baadhi ya zinazoweza kuwa na madhara makubwa na ya muda mrefu kwa wahusika au muhusika mmoja na nyingine madhara yake ni madogo na yasiyo ya muda mrefu.

Wakati wote tunashauri kuachana isiwe ndiyo njia mbadala ya kwanza bali jitihada za kusuluhisha na kubadilika tabia ziangaliwe kwanza na kupewa kipaumbele na kila anayehusika katika penzi.

Kumbuka kuwa katika jitihada za kubadili tabia ni zoezi linalotakiwa kusaidiana baina ya wawili wapendanao na siyo kazi ya mtu mmoja. Nakutakia kufanikiwa zaidi katika uhusiano yako na sio kukimbilia kuachana.

-Mwananchi

No comments:

Post a Comment

Comments system

Disqus Shortname