Naingia
katika lango kuu la chumba cha kuhifadhia maiti katika Hospitali ya
Taifa ya Muhimbili. Watu wengi wamesimama katika makundi, baadhi yao
wakiwa na sura zilizojaa simanzi.
Wengine wamekuja kuwatafuta jamaa zao waliopotea na baadhi wamekuja kuchukua miili iliyopo.
Mlango
wa pili yapo majeneza matatu ambayo tayari yana miili ya marehemu
ndani, hawa wameshasafishwa, kupambwa tayari kwa kusafirishwa, kuagwa
kisha kwenda kuzikwa.
Kushoto
kuna njia ndogo inayoelekea yalipo majokofu ya rangi ya fedha. Simanzi
imetawala katika eneo hilo lenye harufu ya mauti, kwani humu ndimo
ilimolala miili ya marehemu, ambao wanaweza kuwa ni ndugu, jamaa na
marafiki zetu.
Katika njia hii kushoto, kuna chumba, humu wapo wanaume watatu wanamsafisha maiti mwenye jinsi ya kiume.
Amelala katika sinki, mpira wa maji ukimimina maji juu yake, huku mikono ya mmoja wa wanaume, ikimsafisha kwa ustadi mkubwa.
Katika
moja ya dirisha, kuna kitu mfano wa kabati ambacho kimejaa vipodozi vya
kila aina, kuanzia wanja, rangi ya mdomo, mafuta, manukato, mkasi,
viwembe na sabuni.
Mmoja
kati ya watu wanaofanya kazi hii adimu ya kusafisha miili ya marehemu
ni Selemani Uliza anayesema, amesafisha miili ya marehemu kwa miaka 30
sasa.
Anasema
kwa kawaida maiti inapofika huhifadhiwa katika jokofu hadi pale ndugu
watakapofika na kutaka huduma nyingine zaidi ya kuhifadhi.
“Ndugu
huja kumtambua marehemu wao, wakitaka kusafishiwa, basi sisi hufanya
kazi hiyo kwa moyo mweupe tena na kwa ari kuu ya kazi,” anaeleza.
Anasema
kiutaratibu, Hospitali ya Taifa ya Muhimbili hawalazimishi ndugu
kuwatumia wahudumu wa chumba cha maiti kusafisha miili hiyo, bali iwapo
ndugu watahitaji kupata huduma hiyo, basi watalipia na marehemu
atasafishwa.
Gogo
Mzome, Mkuu wa kitengo hiki cha kuhifadhi miili anasema bei iliyowekwa
na Hospitali ya Muhimbili kusafisha miili ya marehemu ni Sh40,000 kwa
maiti moja.
Wanavyofanya kazi
Uliza
anasema wakati wa kusafisha miili hiyo kwanza maiti hutolewa katika
jokofu, baada ya hapo huwekwa katika sinki maalumu ambalo lina bomba na
mpira mwembamba wa kupitisha maji.
Maiti
ikishawekwa vyema katika sinki, bomba la maji hufunguliwa na kwa
kutumia mpira, maiti huanza kuogeshwa na kusuguliwa kwa sabuni na brashi
laini.
“Tunamsafisha
kama binadamu yeyote yule anavyotakiwa kusafishwa, tunamsugua na
kuhakikisha amekuwa safi. Wakati mwingine tunatumia brashi zenye uwezo
wa kutoa uchafu vyema,” anasema.
Baada
ya hapo, anasema maiti hufutwa vyema kwa shuka kisha taratibu
nyingine huendelea iwapo ndugu watahitaji msaada wa aina yeyote kuhusu
ndugu yao.
Kwa
mfano, iwapo ndugu hawawezi kumvalisha marehemu, Uliza na wenzake
humvalisha nguo ambazo zimeletwa kwa ajili ya safari yake hiyo ya
mwisho.
Vilevile,
iwapo ndugu watahitaji marehemu wao apambwe, basi Uliza huifanya kazi
hiyo ambapo kwa kipindi hicho, chumba hiki hugeuka kuwa saluni ya muda.
“Tunampamba
marehemu kwa kutumia kila kifaa ambacho ndugu watahitaji, kwa mfano
poda, kama ni mwanamke lipstiki, wanja na manukato. Kama ni mwanaume
basi tunamvalisha na kumpaka mafuta,” anasema.
Anaongeza
kuwa: “Kama ndugu watahitaji marehemu avalishwe kito cha dhahabu,
huwaita waje kuthibitisha kuwa ndugu yao amevalishwa kito hicho. Unajua
siku hizi binadamu hatuaminiki.”
Baadhi
ya ndugu huamua kuleta vito vya thamani vya ndugu zao kama saa, pete,
au mavazi yao waliyovaa katika harusi ili kuwaenzi au kuwaonyesha
upendo wa mwisho.
Uliza
anasema mbali ya wanawake na wanaume pia husafisha miili ya watoto
wachanga. “Naona kawaida tu ninaposafisha miili hii kwa sababu najua
huyu ni ndugu yangu, na ninapomsafisha, simchukulii kuwa ni mwanamke,
bali marehemu tu wa kawaida,” anasema.
Source: Mwananchi
No comments:
Post a Comment