Maofisa wa ngazi ya juu wa Simba wameanza mazungumzo na kocha Bobby Williamson wa Gor Mahia ya Kenya ili achukue mikoba ya Abdalla Kibaden
SIMBA itaanza mzunguko wa pili wa Ligi Kuu Bara, Januari 26
mwakani dhidi ya Rhino Rangers kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es
Salaam ikiwa na kocha mpya, Mwanaspoti linaweza kuthibitisha.
Maofisa wa ngazi ya juu wa Simba wameanza
mazungumzo na kocha Bobby Williamson wa Gor Mahia ya Kenya ili achukue
mikoba ya Abdalla Kibadeni.
Williamson (52), ni straika wa zamani wa West Bromwich Albion na katika mechi 53 aliyoichezea timu hiyo alifunga mabao 11.
Williamson, ambaye ni raia wa Scotland alijiunga
na Gor Mahia msimu huu na tayari ameipa ubingwa wa Ligi Kuu Kenya ikiwa
ni miaka 18 tangu timu hiyo itwae ubingwa wa Kenya mwaka 1995.
Williamson, ambaye alikuwa kocha wa timu ya taifa
ya Uganda na kuipa ubingwa wa Kombe la Chalenji mara nne, ni kocha
anayesifika kutokana na kufundisha soka la kisasa kwa timu kushambulia
na kukaba kwa pamoja.
Habari kutoka makao makuu ya Simba, barabara ya
Msimbazi jijini Dar es Salaam zinasema kuwa maofisa kadhaa wa klabu hiyo
wameanza mazungumzo na kocha huyo.
Habari hizo zinasema kuwa Simba ina asilimia kubwa
ya kumnasa kocha huyo kwa sababu alikuwa na mkataba wa mwaka mmoja tu
Gor Mahia na kwamba analipwa kidogo.
Simba imeamua kuingiza nguvu zake kwa kocha huyo
baada ya kutoridhishwa na mwenendo wa timu hiyo ambayo inashika nafasi
ya nne katika ligi, lakini kubwa zaidi ni kutokana na benchi la ufundi
kushindwa kudhibiti nidhamu kwa wachezaji na kucheza mpira wa hovyo
uwanjani.
Hakuna kiongozi wa Simba aliyekuwa tayari
kulizungumzia hilo, licha ya karibu wote kukiri kuwa hawaridhishwi na
jinsi timu hiyo inavyocheza.
Williamson aliteuliwa na Shirikisho la Soka Uganda
(Fufa) kuwa kocha wa timu ya taifa ya nchi hiyo ‘The Cranes’ Agosti
19, 2008 akichukua nafasi ya Csaba Laszlo, aliyekuwa amejiuzulu Julai
2008 baada ya kuteuliwa kuwa kocha wa klabu ya Hearts inayoshiriki Ligi
Kuu Scotland.
Akiwa na kikosi cha Uganda, Williamson ameshinda mataji manne ya Kombe la Chalenji mwaka 2008, 2009, 2011 na 2012.
Uganda nusura itinge katika fainali za Mataifa ya
Afrika 2013, lakini ilipoteza mchezo wake wa mwisho wa kufuzu baada ya
kupigiana penalti na Zambia -MWANASPOTI
No comments:
Post a Comment