21 September 2012

Umesalitiwa? Mpenzi wako ni mbinafsi? Hii ndiyo tiba!


INAUMA kusalitiwa, inavunja moyo kuwa mwenzi mwenye hulka za ubinafsi. Unajitahidi kuwa mwaminifu lakini yeye anakwenda kugawa penzi pembeni. Wengine wanaita ‘nje cup’. Unajihimu kushirikiana naye ila yeye anataka afanye mambo yake kivyake.

Kimsingi inauma lakini ndiyo changamoto zilizopo kwenye mapenzi. Uaminifu umekuwa tatizo,
kwa hiyo unahitaji kujengwa ili hali hiyo isikutese. Ukimbaini amekusaliti ujue njia sahihi za kupita kukabiliana na maumivu. Hii ni tiba kamili.

JIFUNZE KUDHIBITI HISIA
Unaposoma makala haya, pengine upo kwenye mateso yanayotokana na maumivu ya kusalitiwa na mwenzi wako au anakuumiza kwa tabia yake ya ubinafsi. Hiyo inakufanya uwe na ujazo mkubwa kichwani wa hisia hasi ambazo zinajumuisha yafuatayo;
    * Hasira
    * Huzuni
    * Wasiwasi
    * Fedheha
    * Maumivu makali kiakili

Kitu sahihi cha kwanza ambacho unatakiwa kufanya ni kuhakikisha unaondokana na maumivu ya kiakili ambayo yanasababishwa na kumbukumbu mbaya za kusalitiwa au matendo yasiyo ya furaha kutokana na jinsi mwenzi wako anavyoonesha ubinafsi.

Baada ya kuondokana na maumivu ya kiakili unaweza kuamua nini cha kufanya kuhusiana na hatma ya uhusiano wako. Inawezekana kupima uzito wa kosa na kufikia mwisho, hivyo ukaachana na mwenzi wako, iwe mchumba, mke au mume.

Unaweza pia kuamua kuketi meza moja na kumaliza tofauti zenu. Ni sawa kwa kile ulichoamua lakini lengo hapa ni kuhakikisha kwamba kumbukumbu za usaliti zinaondoka. Isije mkasameheana halafu siku nyingine katika mazungumzo ukakumbusha: “Unakumbuka siku ile nilikufumania nikakusamehe?”

Ni kosa kuchukua uamuzi lakini wakati huo huo ukabaki na kumbukumbu za tukio la kusalitiwa na mwenzi wako. Iwe unaamua kuachana naye au mnaendelea, hakikisha hubaki na hasira, huzuni, wasiwasi, kujihisi fedheha, kudhalilishwa wala husumbuliwi na maumivu makali kiakili.
Baada ya kuhakikisha hilo umelifanikisha zingatia yafuatayo;

PUUZA NA UYAONDOE MAUMIVU YA KIAKILI
Fikiria kama kuna kitufe kama kwenye kompyuta au simu ambacho ukikibonyeza na maumivu yote yatakwenda na maji. Hivyo basi, unatakiwa uamini kuwa kila kitu kinawezekana, kwa hiyo hupaswi kusumbuliwa na mawazo.

Watu wengi ambao wapo kwenye uhusiano wa kimapenzi na watu ambao ni wasaliti au wabinafsi, wanakabiliwa na maumivu makali ya kihisia. Watu hao wanatamani kusukuma kitufe cha kuwandoa kwenye maumivu lakini kwa bahati mbaya, hicho kitufe hakipo.

Kuna njia ambayo ni sawa na kubonyeza kitufe cha kuondoa maumivu. Ni muhimu kwanza kutambua chanzo cha maumivu. Ukikatiza mitaani, hakuna hata mmoja ambaye anaweza kuhisi maumivu uliyonayo akilini mwako.

Rafiki zako wanaweza kuwa wanajua kwa sababu umewaambia, pamoja na hivyo hawawezi kuwa na utambuzi halisi juu ya kile kinachokutesa. Ni wewe peke yako ambaye unajua kila kitu kuhusu maumivu yaliyomo ndani yako.

Ukiweza kulitambua hilo, maana yake ni kuwa utakuwa umepiga hatua kubwa kukaribia kitufe cha kuondoa maumivu yanayokukabili.  Umeshakaribia lakini hujafikia. Jambo muhimu kufanya ni kuondoa hisia hasi. Ukiwa mbali na hisia hizo, maana yake umepona.

No comments:

Post a Comment

Comments system

Disqus Shortname