13 September 2012

Kura za Yondani zaitoa Simba Ligi Kuu Bara


SAKATA la usajili wa beki Kelvin Yondani, limechuka sura mpya zaidi, ambapo sasa uongozi wa Simba umepanga kujitoa katika Ligi Kuu Bara.
Hatua hiyo ya Simba inakuja kufuatia Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), kupitia kamati yake ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji, kumuidhinisha beki huyo kuichezea Yanga kwa madai kuwa
, kwa mujibu wa kanuni ya 44 kifungu kidogo cha tatu, Yanga ilifuata taratibu za kumsajili.
Akizungumza na Championi Jumatano, Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zakaria Hans Pop muda mchacha baada ya maamuzi hayo, amesema wamelazimika kuchukua uamuzi huo wa kutaka kuiondoa timu hiyo katika ligi, kufuatia kutoridhishwa na jinsi suala la rufaa yao ya kupinga Yondani kuitumikia Yanga, lililovyoshughulikiwa.
Hans Pop amesema wamesikitishwa na hatua ya mwenyekiti wa kamati hiyo ya TFF, Alex Mgongolwa kutaka mfumo wa kupiga kura, ndiyo utumike, badala ya kufuata vifungu vya sheria.
“Kwanza alifanya uamuzi huo (wa kupiga kura) akijua wazi kuwa katika kamati yake kuna wajumbe wengi wenye maslahi na Yanga ambao ni Lloyd Nchunga na Iman Madega ambao waliwahi kuwa viongozi wa juu Yanga pamoja na yeye mwenyewe (Mgongolwa) ambaye ana mapenzi na Yanga.
“Kuna wanachama wetu leo (jana) au kesho (leo) wataenda mahakamani kuishtaki TFF,” alisema Hans Pop na akiongeza:
“Baada ya ya baadhi ya wanachama hao kufungua kesi, sisi pia kama uongozi tunakutana kesho (leo), baada ya kumalizika kwa mchezo dhidi ya Azam. Tunataka kuandaa mkutano mkuu wa dharura kuwaomba wanachama wetu watupe idhini ya kujitoa ligi kuu.
“Likikamilika hilo na lile la kufungua kesi, tunaamini TFF watatufungia kufuatia kupeleka masuala ya michezo katika mahakama za kiraia na baada ya hapo na wao (TFF) watafungiwa na Fifa na hapo ndiyo lengo letu litakamilika la kutaka mpira usichezeke hapa nchini.”

No comments:

Post a Comment

Comments system

Disqus Shortname