19 February 2015

Unalichukuliaje suala la nafasi ya ndugu katika penzi lako!

TAMADUNI za kiafrika, zimeleta athari kubwa sana katika jambo hili, ingawa katika hali ya kawaida, linatazamwa kama ni dogo, lisilo na athari, tofauti na uhalisia wake. Watu wanaliona ni suala la kawaida, la kupuuziwa tu, wakati kiukweli, linatakiwa kutazamwa kwa macho yote.

Kimila, kimazoea na kiutamaduni imetufanya kulifanya jambo hili kuwa la kifamilia. Ndugu wamekuwa na nguvu kubwa katika uhusiano wetu. Ni ngumu kwa mfano, kuwa na rafiki anayeelekea kuwa mke au mume, pasipo uhusika wa ndugu zako. Kama ni msichana, atawajua wifi zake, shemeji zake, wakwe zake na ndugu wengine wa karibu, sawa sawa na itakavyokuwa kwa mvulana, kwani naye ataanza kuonyeshwa shemeji zake, wakwe zake na kadhalika.

Hili ni jambo la kawaida kabisa na linasaidia sana kuboresha uhusiano wa wapendanao. Kwa sababu wapenzi wakishafikia hapa, inapotokea kamgogoro kadogo, ni rahisi shemeji, wifi au ‘mkwe’ kuhusishwa. Mkwe anayehusishwa hapa mara nyingi siyo mzazi moja kwa moja, bali ama huwa baba au mama mdogo na kadhalika.

Ndiyo maana utakuta wawili wamezozana na kesi haraka imefika kwa wifi. Unashangaa dada mtu anampigia kaka au mdogo wake kumuuliza kitu gani kimetokea kati yake na mpenziwe maana amepelekewa mashtaka haya na haya. Inapotokea hivi, ni wazi kuwa mpenzi mmoja ameridhika na mwenzake na ndiyo maana amemfuata ndugu yake wa karibu kwa usuluhishi.

Baadhi ya wapenzi hufikia kiasi cha kuwa na urafiki mkubwa tu na ndugu wa watu wao. Utashangaa kwa mfano, mtu na wifi yake wamekuwa ni marafiki kiasi cha kushangaza, kila mahali wakiandamana na mambo mengi wakifanya pamoja kiasi kwamba kaka mtu anapata wakati mgumu sana katika kutoa maamuzi ya kumuudhi au kumuacha mwenza wake.

Ndugu wa karibu ni muhimu sana katika ujenzi wa penzi la wapendanao, maana kama nilivyosema pale awali, wao ndiyo huwa chachu. Mwanamke hawezi kuwa na amani kama mtu wake hawafahamu ndugu zake, anaona kama hajakamilika hivi. Endapo mwanaume atajaribu kuchengachenga katika kuwafahamu ndugu wa mwenza wake, jambo hili linaweza hata kusabisha mfarakano kati yao.

Lakini wakati tukifahamu fika umuhimu wa ndugu katika uhusiano wetu, ni vema pia kutambua mipaka na nafasi yao kwetu. Kwa sababu wapo baadhi yao, ama kwa kutojua au kwa makusudi, wamekuwa wakiufanya uhusiano wa ndugu zao kuwa wao, kwamba kwa sababu tu yeye ni mama, baba, kaka au dada, basi anataka kuingia hadi chumbani kwenye majadiliano ya migogoro au usuluhushi.

Tunapaswa kuwawekea mipaka ndugu zetu ili kutuwezesha sisi kuwa watu wa mwisho wa kuamua juu ya hatima yetu. Baadhi ya watu hudaiwa kuwa huwa hawakohoi mbele ya mama, baba au kaka zao linapokuja suala la mapenzi. Kama unaendekeza mambo haya, nikushauri uache mara moja. Mama hawezi kukuamulia kuhusu mapenzi yako kwa sababu hajui unachopata au kukosa!

Sisemi kuwa mambo yetu yasiwahusishe ndugu, lakini wao wasiwe ndiyo waamuzi, yaani kauli kama ‘mimi atakavyosema mama ndiyo hivyo hivyo’ hazifai. Wahusishe, lakini waombe wakupe wewe nafasi ya mwisho ya kuamua kuhusu chochote cha maisha yako.

Wewe ndiye unayemfahamu mwenza wako, unajua maisha mnayoishi, unafahamu raha na kero unazopata, unajua kuhusu udhaifu na ubora wake na kila kitu. Sasa asije akaja dada au kaka yako na kukuambia ‘Achana naye huyu, mimi nawajua wanawake/wanaume walivyo’. Kamjulia wapi mtu wako

No comments:

Post a Comment

Comments system

Disqus Shortname