06 November 2013

LOWASSA; NCHI HAINA VIONGOZI JASIRI BALI WALALAMIKAJI. SOMA ZAIDI ALICHOKISEMA HAPA


KIGUGUMIZI cha serikali ya Rais Jakaya Kikwete katika kuchukua uamuzi mgumu kwenye masuala mazito kimemwibua Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, akisema nchi inakosa viongozi jasiri wenye kusimamia utekelezaji wa mambo waliyoamua katika sekta mbalimbali. LOWASSA; NCHI HAINA VIONGOZI JASIRI BALI WALALAMIKAJI 
Alisema nchi ina tatizo kubwa la uswahili mwingi wa kukaa kutekeleza kile kinachotakiwa kufanyika kiasi cha kuwafanya kila mtu kuanza kulalamika.
“Hapa mnaamua bila kutekeleza, watu hawana ujasiri wa kufanya maamuzi magumu, ni lazima awepo mtu mmoja wa kuamua si wote kulalamika lalamika.
“Tukishakubaliana mambo ni lazima yafanyike. Ni lazima tuondokane kuwa nchi ya kulalamika kuanzia kiongozi wa juu mpaka mwananchi,” alisema.
Lowassa aliyasema hayo jana bungeni wakati Bunge lilipokaa kama Kamati ya Mipango ili kujadili Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa mwaka 2014/16.
Lowasa ambaye ni mbunge wa Monduli (CCM) alisema kuwa ni vema serikali ingekuwa na mipango michache yenye kutekelezeka na tija kwa taifa.
Aliongeza kuwa kama angekuwa kiongozi wa serikali angejikita kwenye vipaumbele vitatu ambavyo ni ajira, Reli ya Kati na elimu kuliko kuwa na vipaumbele vingi visivyotekelezeka.
Alibainisha kuwa tatizo kubwa linaloifanya serikali ishindwe kufanya vizuri kwenye maeneo mbalimbali ni kujiwekea vipaumbele vingi huku rasilimali zake zikiwa chache na wakati mwingine zile zinazopatikana hazitumiwi vizuri.
“Vipaumbele vingi mno utekelezaji wake ni tatizo, tungechagua vichache, tukavisimamia na tuvitekeleze. Tukiwa navyo vingi kwa wakati mmoja hatuwezi kuvitekeleza vyote, tuanze na vichache tukivimaliza tunavifuata vingine.
Ajira
Alisema kama angekuwa kiongozi wa serikali angeanza na kipengele cha ajira ambacho kinakwenda sambamba na  mipango.
“Huwezi kupanga bila kuzungumza habari za ajira, tukiri kuna Watanzania wengi wamemaliza kidato nne, sita, chuo kikuu, vyuo, darasa la saba walioko mitaani hawana ajira.
“Tusipowashughulikia, watakula sahani moja na sisi, tusipoangalia yatatufika yale ya wenzetu ya Afrika Kaskazini, si lazima yatufike lakini hawa wasio na ajira watakula sahani moja na sisi,” alisema.
Lowassa aliongeza kuwa wanapaswa kuangalia suala la ajira kwa umakini sana, kwamba inawezekana sana kila mmoja akifanya wajibu wake.
Alibainisha kuwa nchi ya Hispania ilikuwa na tatizo kubwa la ajira mara baada ya kutokea kwa mdororo wa uchumi duniani lakini walikaa chini na kuamua kulitafutia ufumbuzi.
“Wale wenzetu waliamua kila mwekezaji anayekwenda kwao sharti kubwa ni lazima atoe ajira kwa vijana, baada ya miaka miwili walipiga hatua kubwa sana, lazima tuliangalie suala hilo kwa umakini mkubwa sana,” alisema.
Lowassa aliwapongeza Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Fatuma Mwasa na Mkuu wa Wilaya ya Igunga, Elibariki Kingu kwa kuamua kuangalia suala la ajira kwa vijana.
Alisema viongozi hao wamethubutu kwa kuwachukua vijana waliomaliza chuo kikuu na kuwapa matrekta na kuwatafutia ardhi ya kilimo ambapo hivi sasa wanaendesha shughuli zao vizuri.
Aliongeza kuwa Benki ya CRDB nayo imeanza kutoa mikopo kwa vijana wanaomaliza vyuo vikuu kwa kuchukua vyeti vyao kama dhamana.
“Wizara, watendaji na viongozi mbalimbali kila mtu angetimiza wajibu wake katika hili jambo nina hakika tatizo la ajira lingepungua kwa kiasi kikubwa,” alisema.
SHUKA CHINI KUTOA MAONI YAKO

No comments:

Post a Comment

Comments system

Disqus Shortname