16 July 2013

MBOWE ATIWA MBARONI NA KUHOJIWA KWA TUHUMA ZA UCHOCHEZI


MWENYEKITI wa Taifa wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Freeman Mbowe, anashikiliwa na Jeshi la Polisi kwa madai ya kutoa kauli za uchochezi dhidi ya jeshi hilo, vyombo vya dola na serikali kwa ujumla.
Taarifa ya jeshi hilo iliyotolewa na Msemaji wake, Mrakibu Mwandamizi, Advera Senso, imesema kuwa Mbowe amekuwa akitoa kauli ambazo zimekuwa na mlengo wa uchochezi na kuijengea jamii taswira hasi juu ya vyombo vya ulinzi na usalama na kuwafanya wananchi kuwa na hofu.

Mbowe akiandamana na mawakili, Nyaronyo Kicheere na Peter Kibatara, alijisalimisha mwenyewe makao makuu ya polisi majira ya saa 8:30 mchana, mara tu baada ya kuwasili jijini kutoka safarini.


Hatua hiyo imetokana na kitendo cha polisi juzi usiku wa manane kuvamia nyumbani kwake jijini Dar es Salaam na walipomkosa waliacha namba ya simu ya Mkuu wa Upelelezi wa Mkoa wa Kipolisi wa Kinondoni, ili ajulishwe kwamba anahitajika.

Aidha, jana askari wengine kutoka Polisi na wengine wanaoaminika kuwa ni wa Idara ya Usalama wa Taifa walikwenda katika hoteli moja mjini Moshi walikoamini kwamba kiongozi huyo amejificha kwa nia ya kumkamata lakini hawakuambulia kitu.

Mbowe amehojiwa kutokana na uamuzi wa Kamati Kuu ya CHADEMA kutaka kuanzisha kikosi cha vijana cha ulinzi cha Red Brigade na kauli ya kulituhumu jeshi hilo kumjua aliyehusika na bomu lililorushwa kwenye mkutano wa CHADEMA jijini Arusha na kuua watu wanne.

Mwenyekiti huyo pia anahojiwa kwa madai ya kulituhumu Jeshi la Polisi kuisaidia CCM katika uchaguzi mdogo wa madiwani Arusha, pia madai ya kutoa kauli kwamba kitendo cha Rais Jakaya Kikwete kukaa kimya kuhusiana na mauaji hayo, kunaonesha dalili za serikali kujua nani alihusika na tukio hilo.

Tuhuma nyingine ni madai ya kuhamasisha chuki kati ya jeshi na wananchi, pia kuchochea wakazi wa Mtwara katika sakata la gesi.

Mbowe ambaye alihojiwa takriban kwa saa tano, aliachiwa kwa dhamana na anatakiwa kuripoti tena Makao Makuu ya Jeshi la Polisi Julai 23, saa 8 mchana.

Tanzania Daima

No comments:

Post a Comment

Comments system

Disqus Shortname