Mbwana Samatta
SIMBA sasa wamekaa mkao wa kula, kwani mwaka huu ni wa neema kwao.
Kwanza watapata mgawo wa asilimia 20 za mauzo ya straika wao wa zamani,
Mbwana Samatta ambaye ameuzwa katika klabu ya KRC Genk ya Ubelgiji
akitokea TP Mazembe, pili wanasubiri kulipwa Dola 300,000 zaidi ya Sh
600 milioni ambazo wanaidai Etoile due Sahel ya Tunisia.
Katika
mkataba wa Mazembe walipokuwa wanamnunua mchezaji huyo akitokea Simba
uliwataka kuwapa Simba asilimia hizo watakapomuuza klabu nyingine jambo
ambalo limetimia na wanatarajia kupokea Sh 349 milioni kutoka kwenye
mauzo ya Dola 800,000 ambazo mmiliki wa Mazembe, Moise Katumbi amepewa
na Genk huku Samatta akikunja fedha ndefu.
Shirikisho la Soka la
Kimataifa (Fifa) liliiamuru Etoile kuilipa Simba ndani ya siku 60 ambazo
zinakaribia kumalizika na Simba wamegoma kulipwa nusu nusu, wanataka
pesa yao ilipwe kwa wakati mmoja na Etoile wakishindwa kuilipa Simba
watakumbana na adhabu ya kushushwa daraja. Hivyo pesa hizo zikilipwa na
zile za Samatta basi tatizo la ukata kwao litapungua.
Etoile
walimnunua Emmanuel Okwi lakini hawakulipa hata shilingi na baadaye
kuachana naye na Simba kulazimika kufungua kesi hiyo ya madai.
Rais
wa Simba, Evans Aveva amesema kuwa kwasasa wanasubiri kupata mgawo wao
huo na wamepanga pesa hizo kuzipeleka kwenye ujenzi wa uwanja wao uliopo
Bunju B ambao utaanza kujengwa hivi karibuni. Kwa makadirio uwanja wa
mazoezi na uzio wa nyavu unaweza kutumia Sh 150 milioni hivyo pesa hiyo
itatosha kukamilisha ujenzi huo.
“Tunasubiri meneja wa Samatta
arudi maana amekwenda Lubumbashi, ndipo tujue mgawo wetu tunapataje, ila
tumepanga kuipeleka pesa hiyo kwenye ujenzi wa uwanja mzuri kabisa,
fedha za Okwi bado hawajatulipa tunasubiri, muda waliopewa haujaisha,
hatutaki kulipwa nusu tunahitaji fedha,’’ alisema Aveva.
No comments:
Post a Comment