31 January 2016

MAPYA YAIBUKA TANESCO,ZAIDI YA BILION 96 ZATOLEWA KWA AJILI HII


SHIRIKA la Umeme nchini (Tanesco), limesaini mkataba wa Euro milioni 42  ambazo ni sawa na Sh bilioni 96.7 kutoka Wizara ya Uchumi ya Ujerumani kupitia Benki ya Maendeleo ya Ujerumani (KFW), Umoja wa Ulaya na Shirika la Maendeleo la Ufaransa ili kukamilisha mradi wa umeme.
Fedha hizo zitaokoa kiasi cha Sh bilioni 30 kwa mwaka zinazotumika kununulia mafuta katika mradi wa umeme wa mikoa ya Kaskazini Magharibi mwa Tanzania.
Hayo yamesemwa jana na Mkurugenzi Mkuu wa Tanesco, Felichesmi Mramba, baada ya kusaini mkataba huo.
“Mradi huo utaunganisha mikoa mitatu ambayo ni Geita, Kagera na sehemu nyingine za Kigoma, hivyo ujenzi utakuwa wa 220Kv zitakazotoka Geita hadi Nyakanazi ambayo inakadiriwa kuwa na urefu wa kilomita 144,” alisema Mramba.
Mramba alisema mradi huo utawezesha kujengwa kwa vituo vipya vya kupoza umeme vya Nyakanazi, Biharamulo, Chato na Kakonko ili kukidhi mahitaji ya wakazi wa eneo hilo.
“Mradi huu utasaidia kupunguza gharama za uzalishaji na usambazaji umeme katika mikoa ya Kaskazini Magharibi mwa Tanzania hivyo kusaidia kuboresha maisha ya wakazi wa eneo husika na kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla,” alisema Mramba.
Alisema Ujerumani kupitia KFW ilikubali kutoa msaada wa Euro milioni 20 ambazo ni sawa na Sh bilioni 46 za Tanzania na AFD itatoa mkopo wa Euro milioni 14 ambazo ni sawa na Sh bilioni 32.5 za Tanzania.
Kwa upande wake mwakilishi wa umoja wa Ulaya, Eric Beaume, alisema mradi huo ni moja kati ya iliyoonyesha ni namna gani umoja huo ulivyojizatiti kuhakikisha maisha ya mtu mmoja mmoja yanabadilika kupitia nishati ya umeme.
Alisema mradi huo utasaidia kaya 10,000 katika vijiji vya mikoa iliyotajwa na taasisi za afya, shule na vituo vya polisi.

No comments:

Post a Comment

Comments system

Disqus Shortname