SHIRIKA la Umeme nchini (Tanesco), limesaini mkataba wa Euro milioni
42 ambazo ni sawa na Sh bilioni 96.7 kutoka Wizara ya Uchumi ya
Ujerumani kupitia Benki ya Maendeleo ya Ujerumani (KFW), Umoja wa Ulaya
na Shirika la Maendeleo la Ufaransa ili kukamilisha mradi wa umeme.
Fedha hizo zitaokoa kiasi cha Sh bilioni 30 kwa mwaka zinazotumika
kununulia mafuta katika mradi wa umeme wa mikoa ya Kaskazini Magharibi
mwa Tanzania.
Hayo yamesemwa jana na Mkurugenzi Mkuu wa Tanesco, Felichesmi Mramba, baada ya kusaini mkataba huo.
“Mradi huo utaunganisha mikoa mitatu ambayo ni Geita, Kagera na
sehemu nyingine za Kigoma, hivyo ujenzi utakuwa wa 220Kv zitakazotoka
Geita hadi Nyakanazi ambayo inakadiriwa kuwa na urefu wa kilomita 144,”
alisema Mramba.
Mramba alisema mradi huo utawezesha kujengwa kwa vituo vipya vya
kupoza umeme vya Nyakanazi, Biharamulo, Chato na Kakonko ili kukidhi
mahitaji ya wakazi wa eneo hilo.
“Mradi huu utasaidia kupunguza gharama za uzalishaji na usambazaji
umeme katika mikoa ya Kaskazini Magharibi mwa Tanzania hivyo kusaidia
kuboresha maisha ya wakazi wa eneo husika na kukuza uchumi wa mtu mmoja
mmoja na taifa kwa ujumla,” alisema Mramba.
Alisema Ujerumani kupitia KFW ilikubali kutoa msaada wa Euro milioni
20 ambazo ni sawa na Sh bilioni 46 za Tanzania na AFD itatoa mkopo wa
Euro milioni 14 ambazo ni sawa na Sh bilioni 32.5 za Tanzania.
Kwa upande wake mwakilishi wa umoja wa Ulaya, Eric Beaume, alisema
mradi huo ni moja kati ya iliyoonyesha ni namna gani umoja huo
ulivyojizatiti kuhakikisha maisha ya mtu mmoja mmoja yanabadilika
kupitia nishati ya umeme.
Alisema mradi huo utasaidia kaya 10,000 katika vijiji vya mikoa iliyotajwa na taasisi za afya, shule na vituo vya polisi.
No comments:
Post a Comment